|
MAKABURI YA HALAIKI -ZANZIBAR
Idadi hasa ya wazanzibari waliokuwa katika Mapinduzi haijulikani. Inakisiwa tu kuwa ni kiasi ya watu 2,000 hadi 20,000. Hata hivyo, kilicho bayana ni kuwa idadi ya wahanga - miongoni mwa jeshi la serikali na lile la Mapinduzi ilikuwa ndogo mno. Kiongozi wa Mapinduzi hayo anaripoti kuwa alipokea taarifa ya wahanga hao tarehe 13 Januari, saa 9:30 alasiri baada ya sultani kukimbia na vikosi vyote vya serikali kwisha kushindwa. Anaadika kuwa katika ushindi wao wa Zanzibari - yaani ule wa ghala ya silaha na ule wa vikosi vya serikali - upande wake ulipoteza askari 2 na kujeruhiwa wengine 18. Ama kwa upande wa serikali, katika mapigano haya mawili yaliyopishana kwa takribani masaa 2, majeshi 16 waliuawa na 81 wakaachwa majeruhi. Wakati wa kuziteka ngome nyengine za serikali asubuhi hiyo, mauaji zaidi yalitokea. Hata hivyo, hisabu ya jumla ya wahanga wote katika "medali ya vita", ikijumuisha na ya ziwani, ilikuwa ni askari 9 tu waliouawa na 173 tu walijeruhiwa kwa upande wa jeshi la Mapinduzi,na 70 tu waliouawa na 401 walijeruhiwa kwa upande wa vikosi vya serikali. Askari na wapiganaji wengine 818 wa serikali walijisalimisha aidha wakati ama baada ya mapambano. Idadi hii ya wahanga 653 tu miongoni mwa waliouawa na waliojeruhiwa, kwa pande zote mbili, hailingani kabisa na ile idadi ya maelfu ya wahanga waliopoteza maisha, viungo katika pirika-pirika za muendelezo wa Mapinduzi.
"Vita ni dhamana ya kuogofya na matokeo yake daima ni uharibifu mkubwa. Hakuna chochote kiwezekanacho kuthibitisha hili zaidi ya vita vilivyotokea tarehe 12, Bubwini Kaskazini Unguja, eneo ambao waliishi waarabu wengi. Eneo hili lilikuwa ni kituo cha kuhifadhia silaha ambazo waarabu hawa walikusudia kuzitumia katika mauaji ya maangamizi dhidi ya waafrika. Kwa hakika walipanga kufanya shambulizi hilo siku ya tarehe 13 Januari. Nilipata habari hizi kutoka kwa kijana aliyekuwa karibu kuuawa na wanajeshi Wazungu. Wanajeshi hawa walikuwa tayari wameshawaua watu 40 katika eneo hilo na nilikuwa na bahati ya kuwasili hapo wakiwa wanataka kummaliza kijana huyu kwa risasi. Nilipomsaili zaidi, kijana huyu aliniambia kuwa silaha zilikuwa zimehifadhiwa katika eneo hili na waarabu walishapanga kuzitumia hivi punde tu; pia aliniambia kuwa wengi miongoni mwa wale waliouawa na askari wazungu hawakuwa wakaazi wa nyumba walizokutwa. Habari hizi za uovu zilithibitisha habari nilizozipata hapo kabla na nilichukizwa sana. Niliwaamuru askari wangu wafyatue risasi kila upande na wakiuwe kiumbe chochote kilicho mbele yao- wanaume, wanawanake, watoto, walemavu na hata kuku na mbwa"
Siku mbili baada ya Mapinduzi, mpiga picha wa kitaliano alipiga picha zilizozaa makala hii. Picha hizo zinaonesha misururu mirefu ya wafungwa, watu wakikimbia kupitia pwani, maiti waliozagaa ufukweni, mauaji ya wafungwa, usafishwaji wa miili ya wahanga na makaburi ya halaiki.
Makala hii imeandikwa kama ni kumbukumbu ya wale wote waliopoteza maisha yao wakati wa Mapinduzi. Na Barghash 2001 Barghash@msn.com |